UPATANISHO WA KISARUFI KATIKA KISWAHILI

ALCHERAUS R. MUSHUMBWA, 2018

1. Maana ya upatanisho wa Kisarufi
Kwa mujibu wa BAKITA (2015:1107), upatanisho wa kisarufi ni kukubaliana kisarufi kunakojitokeza kati ya nomino kiima na kitenzi au na kivumishi kunakobainishwa na viambishi. Kwa mwongozo huo, tunafasili patanisho wa kisarufi kuwa ni kukubaliana kisarufi kunakojitokeza kati ya nomino kiima na kitenzi; au, na kivumishi kunakobainishwa na viambishi. Kukubaliana huku huwa kunahusisha nomino mtenda au mtendwa, kiwakilishi, kivumishi na kitenzi kwenye mpangilio sahihi wa sentensi za Kiswahili. Hii ina maana kuwa viambishi (awali) vinavyoambikwa kwenye kivumishi au kitenzi katika sentensi huzingatia aina ya nomino mtenda au kiwakilishi chake au nomino mtendwa kwa sababu nomino mtenda au mtendwa kwenye tungo za Kiswahili huwa ndiyo mhusika anayetolewa taarifa katika tungo husika. Viambishi vya upatanishi wa kisarufi katika Kiswahili sanifu huteuliwa kulingana na aina na pia kundi (ngeli) la nomino mtenda au mtendwa inayoarifiwa. Lengo la upatanisho wa kisarufi ni kuleta maana sahihi na yenye mantiki kwa wazungumzaji.

Utokeaji wa Upatanishi wa Kisarufi
Upatanishi wa kisarufi katika tungo za lugha ya Kiswahili hutokea kwenye vipashio mbalimbali vinavyounda tungo husika kulingana na taratibu za kisarufi (Mhilu na Masebo, 2010:1-2).
a)      Nomino na Kivumishi (N+V)
Mizizi ya vivumishi vya Kiswahili huchukua viambishi vya upatanisho kulingana na nomino inayovumishwa ipo katika kundi lipi kwa kuzingatia umoja na wingi ili kuleta uafikiano. Kwa mfano:
1.      Mtu mwema (umoja)/ Watu wema (wingi)
Mbwa mzuri (umoja)/ Mbwa wazuri (wingi)
2.      Kitabu changu (umoja)/ Vitabu vyangu (wingi)
Kiti kirefu (umoja)/ Viti virefu (wingi).

b)      Nomino na kitenzi (N+T)
Upatanisho huu unahusisha nomino mtenda katika tungo pamoja na viambishi awali vinavyoambikwa kwenye mzizi wa kitenzi ili kuleta ukubalifu wa tungo kimuundo. Kitenzi (mzizi) hulazimika kuchukua kiambishi awali kinachoendana na nomino mtenda kwenye tungo ambapo kiambishi hicho hutambulika kulingana na nomino iko kwenye kundi lipi la majina katika umoja na wingi. Kwa mfano:
1.      Uovu umezidi mtaani kwetu (umoja)/Maovu yamezidi mtaani kwetu (wingi)
2.      Mto umekauka (umoja)/Mito imekauka (wingi)



c)      Nomino, kivumishi na kitenzi (N+V+T)
Katika mpangilio huu wa tungo, upatanisho wake huwa ni ukubalifu wa mpangilio sahihi wa vipashio (nomino mtenda+kivumishi+kitenzi) ambapo kivumishi (mzizi wake), na kitenzi (mzizi wake) hukubali kuchukua viambishi awali vinavyoitabulisha nomino mtenda kwenye tungo hiyo. Upatanisho huu nao hufuata utaratibu wa kuzingatia aina ya nomino na kundi lake inamojumuishwa katika makundi ya majina. Kwa mfano:
1.      (a) Ukuta ule umebomoka (umoja)/Kuta zile zimebomoka (wingi)
(b) Ukuta wangu umebomoka (umoja)/Kuta zangu zimebomoka (wingi)
(c) Ukuta mzuri/mrefu umebomoka (umoja)/Kuta nzuri /ndefu zimebomoka (wingi)
2.      Kucheza kwake kunachosha.

d)     Kitenzi na nomino mtendwa (T+N-mtendwa)
Hapa upatanisho hutokea pale kitenzi kinapotangulia jina au nomino ambayo ndiyo huwa imeathirika na tendo. Kiambishi cha upatanisho wa mtendwa huwa katika kitenzi na kiambishi hicho huwa ndicho kiwakilishi cha nomino hiyo kwa utaratibu wa kuzingatia kundi ambalo nomino hiyo imo. Kwa mfano:
1.      Umemtuma Juma dukani? (umoja)/Umewaita watoto wale? (wingi)
2.      Ameikata kamba yangu (umoja/Amezikata kamba zangu (wingi)

e)      Kiwakilishi na Kivumishi (W+V)
Kiwakilishi ni neno linalochukua nafasi ya nomino au jina katika sentensi. Hivyo, bila kuwepo nomino basi nafasi yake inachukuliwa na kiwakilishi. Upatanishi wa kisarufi pia huvikumba viwakilishi vya Kiswahili pale vinapofanya kazi ya nomino mtenda au mtendwa katika tungo. Kwa hiyo, upatanishi wa kiwalikishi na kivumishi ni pale kivumishi (mzizi wake) kinapokubali kuchukua kiambishi awali kinachowakilisha kiwakilishi ili kuleta ukubalifu wa kimuundo kwenye sentensi. Kwa mfano:
1.      Mimi mfupi sana (umoja)/Sisi wafupi sana (wingi)
Huyu mnene kabisa (umoja)/Hawa wanene kabisa (wingi)
2.      Hiki chembamba (umoja)/Hivi vyembamba (wingi)
Kile kifupi (umoja)/Vile vifupi (wingi)

f)       Kiwakilishi na kitenzi (W+T)
Kitenzi kinachoandamana na kiwakilishi kwenye tungo, mzizi wake huambikwa kiambishi awali kipatanishi kinachoiwakilisha nomino inayowakilishwa na kiwakilishi hicho ili kuleta uafikiano wa vipashio hivyo kwenye tungo. Ifuatayo ni mifano ya upatanisho wa kisarufi kati ya Kiwakilishi na Kitenzi:
1.      Hili limeharibika (umoja)/Haya yameharibika (wingi)
Zuri limeharibika (umoja)/Mazuri yameharibika (wingi)
2.      Ule umekatwa (umoja)/Ile imekatwa (wingi)
g)      Kiwakilishi, kivumishi na kitenzi (W+V+T)
Katika upatanisho huu, kivumishi na kitenzi vinavyoandamana na kiwakilishi ili kuunda tungo, hulazimika kupokea viambishi awali vya upatanishi vinavyowakilisha nomino mtenda inayowakilishwa na kiwakilishi kilicho katika tungo husika ili kuleta uafikiano au ukubalifu sawia. Kwa mfano:
1.      Langu lile limepotea (umoja)/Yetu yale yamepotea (wingi)
2.      Kimoja kidogo kimenunuliwa (umoja)/Vingi vidogo vimenunuliwa (wingi)

h)      Kitenzi na kiwakilishi (T+W)
Hapa, tungo huwa inahusisha kitenzi na kiwakilishi ambapo kitenzi hutangulia kiwakilishi cha nomino mtendwa. Upatanisho wake huwa ni pale ambapo kitenzi hubeba kiambishi cha upatanisho wa kisarufi ambacho huiwakilisha nomino mtendwa inayowakilishwa na kiwakilishi. Kawa hiyo, ili tungo ilete mantiki na ukubalifu sahihi inabidi kitenzi kikubali kupokea kiambishi cha upatanisho kinachowakilisha kiwakilishi cha nomino mtendwa. Kwa mfano:
1.      Amepigwa yeye mwenyewe/Wamepigwa wao wenyewe
Nimetumwa mimi/Tumetumwa sisi
2.      Kimenunuliwa kirefu/Vimenunuliwa virefu
Hadi kufikia hapa, angalau kwa kiasi, dhana ya upatanishi wa kisarufi katika lugha ya Kiswahili imeelezewa na kupata picha halisi ya jinsi upatanishi wa kisarufi huchukua nafasi kwenye lugha ya Kiswahili. Aidha, kinachoweza kuelezwa kwa ufupi ni kwamba kinachoongoza kanuni ya upatanishi wa kisarufi ni mlengwa mkuu katika tungo – yaani, nomino mtenda au mtendwa kama ilivyodhihirishwa kwenye ufafanuzi na mifano yake. Kanuni inayoongoza upatanishi wa kisarufi inasema kuwa nomino mtenda au mtendwa pamoja na kiwalikishi chake itawakilishwa katika kivumishi au kitenzi kinachoandamana nayo kwenye tungo kwa umbo au maumbo (viambishi) yanayoitambulisha nomino hiyo kulingana na umilikwaji wake kwenye kundi au ngeli za majina.” Kwa maana hii basi, kinachofanya utambuzi wa kupachika viambishi vitakavyoleta upatanishi kwenye tungo ni yale maumbo yanayoiwakilisha nomino husika kwenye ngeli au kundi inamomilikiwa. Kanuni hii hutambuliwa na watumiaji wa lugha ya Kiswahili kwenye akili zao pale wanapokuwa wanazungumza au kuandika kwa lengo la kuwasiliana. 

MAREJEO
BAKITA,Kamusi Kuu ya Kiswahili (KKK), Dar es Salaam: Longhorn Publishers Limited,
               2015.
Mhilu, Greyson na Masebo J. A, Kiswahili kwa Shule za Sekondari Kidato cha Tatu, Dar es
            Salaam: Nyambari Nyangwine Publishers, 2010.
Mlyauki, Justa, E. mulashani na D. Ndilime, KiswahiliKitukuzwe 3, Malaysia: Pearson
              Education Limited, 2009.


0 maoni:

Copyright © 2012 JUKWAA LA KISWAHILI - Blogger Theme by SoraTemplates