Shairi natunga
Nami natunga shairi, yamoyoni kuyasema
Kweli ni vema kukiri,bayana ni jambo jema
Mungu wala si bakari,waja hujalia mema
Kayasema sulutani manenowe ni sheria.

Heri njiwa kununua,kuliko  wale watumwa
Bora kazi kuibua,wao mbele kusukumwa
Njaazo kusisimua,zingoje tunda kuchumwa
Kayasema sulutani,manenowe ni sheria.

Mara ya mia elimu,bure na ipatikane
Shida zao hao walimu,subiri tutulizane
Wakinena mahasimu,wamejambatuuchune
Kayasema sulutani,manenowe ni sheria

Zinjengwe kwanza njia, wajenzi leo wasile
Punda afe nasikia,zege katu lisilale
Wengi wanamlilia,tabu zao tangu kale
Kayasema sulutani,manenowe ni sheria.

Watumwa mlo wakila,Kazi nzuriwatachapa
Na sulutani kalala,hataki haki kuwapa
Kuwanyima wao kula,sote twatapatapa
Kayasema sulutani,manenowe ni sheria.

Shime nawausieni,enyi Watumwa wa heri
Kazi daima chapeni,kudai sio hatari
Sauti zenu pazeni,madai  yawe habari
Kayasema sulutani,manenowe ni sheria.

©sir manyuka

0 maoni:

Copyright © 2012 JUKWAA LA KISWAHILI - Blogger Theme by SoraTemplates