HADITHI FUPI

*Kiu ya Chuo*
Akiwa ameketi  katika mkeka mchafu  uliotandikwa chini ya   Mfenesi alijikuta akitililikwa na machozi mithili ya mtu aliye fiwa.Hata hivyo machozi hayakufifisha mvuto wa macho ya kimahaba ya Sikujua. Sikujua alikuwa binti mrembo wakuvutia,urefu na unene wake wa wasitani,miguu mizuri iliyounganishwa na mapaja manene ambayo yalishikilia barabara makalio makubwa vilimfanya arushe roho za marijali.Kiuno cha Sikujua kilijikata vema,tumbo dogo na chuchu za saa sita mchana zilipamba kifua cha kigori huyu.Shingo yake ilikamatilia sawasawa kichwa chenye nywele ndefu.Uso wa duara rangi ya Maji ya kunde ulionakishiwa na puwa ndefu ndefu,macho   na mdomo mdogo vilikamilisha umbile timamu la Sikujua.
"Bibie vipi watokwa na machozi?!"nilihoji huku nikimtazama kwa jicho lakipekuzi.
" Kaka yangu dunia si yangu tena,kila kitu kimesambaratika sina kesho yangu nimevurunda kila kitu kaka yangu" Sikujua alijibu huku akigugumia kwa kwikwi ya kilio.
"Bado umeniweka gizani dada yangu,nieleze kipi hasa kilichokusibu?" niliendelea kumsaili.
"Kiu ya Chuo imenitokea puani"
"Kivipi Dada?"
"Kaka niliamini mwisho mwema hutakatisha njia kumbe la ,njia sahihi ndio huleta mwisho mwema." Alijibu huku akijifuta machozi kwa kitambaa.
"Unazidi kuniweka njia panda Sikujua"nilidodosa.
Basi Sikujua anza kunisimulia."Mimi nimezaliwa katika familia duni,baba ni mkulima wa bustani ya nyanya na vitunguu.Mama ni fundi mfinyazi wa vyungu.Kipato cha nyumbani ni cha kulenga na manati,kula yetu yenyewe moja kwa kutwa.Nakumbuka enzi nasoma shule ya msingi mama alikuwa akinipikia viazi au mihogo na wakati mwingine Matoborwa jioni, na asubuhi aliniwekea katika mkoba wa shule.Ilikuwa ni utaratibu wa kila siku kubeba chakula cha kula mchana kwani hapa kuwa na fedha ya kunipa ili ninunue chakula niwapo shule.Nilisoma kwa tabu sana kaka yangu.Nguo za shule nilinunuliwa Mara moja kila baada ya miaka miwili.Mama alikuwa akinishonea kwasindano ya mkono na uzi wa sandarusi kuziba matobomatobo katika sare zangu za shule.Hali ya maisha ya wazazi wangu imekuwa ngumu kwa muda mrefu sana.Baba anapokosa fedha ya kununulia chakula huwa hana budi kutafuta kibarua chochote ili sisi familia yake mikono iende kinywani.Kilimo chake cha nyanya ni duni hana mtaji wakutosha,pembejeo ni duni na wala hakuna cha  bwana shamba wala bibi shamba hivyo baba anafanya Kilimo cha kienyeji sana.
Pamoja na milima na mabonde yote niliyokuwa na kutana nayo katika safari yangu ya kielimu nilijikaza hatimae nikafanikiwa kujiunga shule ya sekondari.Sitasahau Furaha niliyoipata siku ile napewa taarifa kuwa nimechaguliwa kujiunga kidato cha kwanza katika shule ya sekondari Tembo." Hongera sana Sikujua umefaulu na umechaguliwa kujiunga Tembo" ilikuwa ni sauti ya Mwalimu Sijaona.Moyo wangu ulilipuka kwa furaha hali iliyofanya mwili wangu kusisimuka kutokana na hisia tamu za burudiko lilomea nafsini mwangu.Taarifa za kufaulu kwangu kwa wazazi wangu zilileta furaha iliyochanganyikana na hofu.Hofu ya wazazi wangu ilikuwa ya kimsingi kabisa baba alijikuta njia panda; kunipeleka shule au kukacha.Ada ya shule na michango mingine pamoja na sare za shule ilikuwa mtihani mzito." Mwanangu umefaulu hongera,lakini tutafanyeje sasa ikiwa kula yenyewe inatushinda?!,samahani mwanangu",maneno ya baba yalinichoma mkuki moyoni kwani haya kuwa ya matumaini kabisa.Furaha yangu iligeuka huzuni ghafla.Lakini mama alimtia moyo baba." Baba Sikujua usiseme hivyo unamkatisha tamaa mwanao,kashatutoa kimasomaso wazazi wake.Ni wajibu wetu kuhakikisha anakwenda shule,huwezi jua huyu anaweza kuwa mkombozi wetu wa baadae.Hebu tazama tangu tukiwa vijana hadi sasa uzee unatunyemelea bado ufukara unatuadhibu! Kilichobaki sasa tufanye chochote kumwendeleza mwanetu kipenzi wapekee."Mama alirejesha tumaini langu.Baba alipumua kwa nguvu ahuuu!kisha akanishika bega la kushoto mwanangu nakupenda sana nitafanya lolote liwezekanalo kukusomesha hadi ufikie ndoto zako.Mama yako na mimi tu nakutegemea wewe.Wewe Sikujua kuanzia sasa ni tumaini letu.Sikujua..! aliniita huku akinitazama usoni.Labeka baba! Nilitika.Wewe ni Tumaini.Baba aliongea kwa msisitizo.Tangu hapo nilianza kusoma kwa bidii sana.Nilielewa wazazi wangu waliamini Mimi ndio n itakuwa msaada wao kwa baadae na ili niweze kuwa tumaini la kweli la wazazi wangu hapakuwa na budi kufaulu mtihani wa kidato cha nne.Nilijijengea nidhamu,niliwaheshimu walimu nao wakanipenda.Jembe halimtupi mkulima kaka hatimae nilifaulu na kujiunga kidato cha tano ambako nako nilifanikiwa kufanya vizuri katika mtihani wa kidato cha sita.Kiu yangu kuu ulikuwa ni kusoma Chuo kikuu,ndoto yangu ni kuwa dakitari lakini...lakini...ni..ni..nikama nimepoteza kila kitu! Sina thamani tena,nimewaangusha wazazi wangu.Mimi sio Tumaini."Sikujua alijikitu machozi na kilio kikuu vikimkaba koo akakosa la kuongea zaidi ya kumwaga kilio cha kusaga na meno.Nami niliamua kumwacha alie ili kutoa hisia za maumivu aliyokuwa nayo.Tayari niling'amua bila shaka kuwa Sikujua alikuwa amekabiliwa na masaibu makubwa.Kwa wakati ule ilifaa kumwacha alie kisha akinyamaza mazungumzo yaendelee.Taaluma ya ualimu niliyosomea hasa somo la ushauri nasaha lilinisaidia sana.Wakati Sikujua unaendelea kulia nikajiahidi kumsaidia kwani tiba ya tatizo lake ni usadi tu."Hapa ushauri nasaha unahitajika" nilijisemea moyoni.
Baada ya kitambo kidogo Sikujua alinyamaza kulia.Mazungumzo yetu yakaendelea."Sikujua nini kimetokea hata usiwe Tumaini tena?!"nilihoji."Kaka yangu nilipohitimu kidato cha sita hali ya kiuchumi nyumbani ikawa mbaya zaidi ya mwanzo baba anaumwa madonda ya tumbo hawezi tena kufanya kazi ngumu.Mama ndo anahudumia familia.Kipato cha mama ni kidogo hakiwezi hata kukidhi mahitaji muhimu nyumbani.Ufukara umevamia familia yetu.Baba anahitaji fedha ya matibabu mimi nahitaji fedha ya ada ya Chuo."Sasa si ungeomba mkopo wa serikali?"  nilimuuliza Sikujua huku nimemkodolea macho."Kaka yangu niliomba lakini sikufanikiwa,siku ya kufa nyani miti yote huteleza."Sikujua alisisitiza."Duh! Hii nchi nayo inamaajabu yake,ama kweli ukisitaajabu ya Mussa utayaona ya Firauni;hivi inawezekanaje ukose mkopo ilihali watu wanaotoka familia bora wanapewa?!."nilijikuta nikimuuliza swali ambalo lilikuwa nje ya uwezo wake."Ndo hivyo kaka yangu.Baada ya kuona hivyo ikanibidi niende mjini kutafuta japo kijikazi cha kuniingizia kipato cha kujikimu.Mjini nako mambo hayakuniendea vizuri kwani nilitanga huku na kule bila kupata kazi ya maana hatimae nikaamua kufanya kazi baani! Yaani kaka yangu..." Sikujua alishindwa kumalizia badala yake alianzakulia tena.Awamu hii nilichukua kitambaa changu na kuaanza kumfuta machozi yaliyokuwa yakitiririka mashavuni pake mithili ya maji ya bomba.Kisha akaendelea;Kazi ya kuuza vinywaji inachangamoto zake.Kwanza unafanyakazi hadi usiku wa manane, ujira kidogo, kero za walevi na hatari ya vishawishi.Nilijitahidi kuvumilia yote ili tu niweze kupata chochote kitu nijikimu na kumusaidia mama kutunza familia nyumbani.Siku moja  nikiwa kazini alifika mteja mmoja aliejiita Sijali na kuomba nimuhudumie.Bwana sijali alikuwa ni mtu wa makamo apatae miaka arobaini hivi,ni mtu alieonekana kujiweza kifedha.Kwa nje alionekana mtu mpole, mcheshi na mwenye huruma lakini kumbe ni mkatili asie na mfano.Sijali ameniachia donda ndugu, ameyafanya maisha yangu yakose thamani yaani sikujua kama Sijali angenifanyia hivi.Upole na usikivu aliouonesha Sijali kwa nje ulinilaghai akili nikaamini angeweza kunisaidia.Nilimsimulia mkasa wa maisha yangu na ya familia pamoja na kiu yangu ya chuo.Sijali aliniahidi kunisaidia siku hiyo aliniachia namba ya simu akinisistiza nimtafute kesho yake ili anielekeze atakapokuwa ili tukutane na aone jinsi ya kunisaidia.Kesho yake ilipofika nilimtafuta na akanielekeza alipo nilienda lakini chakushangaza nilimkuta peke yake nyumbani nilipo muuliza alidai mkewe na watoto walikuwa wamesafiri.Alinikaribisha sharubati iliyo kuwa imejaa katika bilauri ndefu, nilishukuru kisha nikaanza kunywa.Kaka yangu sikujua kilichoendelea baada ya hapo badala yake ilikuwa ni kufumba na kufumbua nikajiona nipo chumbani kwake na bwana Sijali sote tukiwa uchi wa mnyama.Kitanda tayari kilikuwa kimesambaratika hali iliyo onesha dhahiri kuwa kazi aliyokusudia Sijali ilikuwa imekamilika.Si kuwa na la kufanya zaidi ya kulia kilio kisicho na msaada.Sijali alikuwa kimya akinitazama tu.Niliamua kuvaa nguo na kuondoka lakini kabla sijafika mbali aliniita; "Sikujua tafadhali simama". Nilisimama." Tafadhali shika zawadi yako".Sijali alinipatia bahasha ya kaki,wala Sikujua kulikuwa na zawadi gani ndani ya bahasha ile kwa wakati ule hadi nilipo fika nyumbani na kuifungua.Nilipofungua sikuamini macho yangu,kulikuwa na vipande viwili vya karatasi kimoja kilikuwa ni hundi ya milioni tatu na cha pili kilikuwa na ujumbe wa maneno uliochoma moyo wangu.Ujumbe ulisema: "Sikujua Mimi Sijali ndoto za mtu nacho jali Mimi ni adhima yangu ya kukidhi haja zangu.Hata hivyo nimekupenda nimeaamua nikusaidie hiyo fedha ukasome ili ukate kiu yako ya chuo.Napenda utambue wazi pia Mimi sio mzima kwahyo wewe pia kwa sasa si mzima.Mimi na wewe tuna Virusi vya Ukimwi. Wengi nimewaambukiza lakini Sijali, kwani nani ajuae kuathirika kwangu? Niliambukizwa na wanawake nami lazima niwaambukize.Pole Sikujua kwa kuwa miongoni mwa orodha yangu." ....Sikujua hakuendelea tena kusimulia kwani kwikwi na kilio kilimzidi.Nilimwacha hadi aliponyamaza mwenyewe ndipo nilipo anza kumtia moyo dada yangu huyu wa hiyari.Ukimwi sio mwisho wa maisha,ipo njia ya kuishi kwa matumaini.Kinachotakiwa nikupiga moyo konde maisha lazima yaendelee na ndoto sharti kuifikia.Zote ni changamoto za maisha kuzikabili hakuna budi.Mazungumzo yangu na Sikujua yalikuwa ni tiba kwake alitoa sumu zote akawa salama kihisia. Tangu siku hiyo hadi sasa Sikujua ni mtu mwenye furaha maishani.Mwaka uliofuata alipata ufadhili wa masomo toka shirika fulani la kidini akaenda kusoma udaktari chuo kimoja nchini Ujerumani.Aliporejea kaanza kufanya kazi yake vizuri.

Mtunzi: Manyuka, M.K
Mawasiliano: 0764419640/ manyukakapaya@gmail.com

Maoni 1 :

  1. Pata mkopo wako sasa ndani ya masaa 48

    Siku njema

    Je! Unataka kuwa mjasiriamali, kuanza mradi au kununua nyumba au wewe ni katika kurekebisha fedha, msaada wako unakuja sasa, umepoteza ndoto yako, kujaribu kupata tayari, usiruhusu ndoto zako kufa, wasiliana na Mr. Fred zaidi, kwa mkopo wa haraka na wa kuaminika.

    Tunatoa aina hii ya mkopo chini:

    Mkopo wa biashara 1

    biashara
    mkopo wa tatu ghorofa

    mkopo 4. auto

    mkopo 5. mkopo wa mkopo, nk.

    Tunatoa mikopo kwa wateja wenye dhati na waaminifu ambao wako tayari kushirikiana nasi na kiwango cha riba cha 3%, kuanzia 100,000.00 hadi 500,000,000,000.00.

    Wasiliana nasi haraka kupitia e-mail yetu (fredmorefinance@gmail.com)

    (fredmorefinance@hotmail.com)

    Nambari ya Whatssap: +919654763221

    Iliingia

    Mkurugenzi

    Mheshimiwa Fred zaidi

    JibuFuta

Copyright © 2012 JUKWAA LA KISWAHILI - Blogger Theme by SoraTemplates